Waziri Mkuu ataka Uwajibikaji anuwani za makaazi
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa ameagiza Wizara zinazohusika na Zoezi la Anwani na Makazi kutatua Changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika Zoezi hilo.
Mhe. Majaliwa ambae ni Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya Taifa ya Sensa ya watu na Makazi ameyasema hayo katika kikao cha Tano Cha Kamati hiyo pamoja na Tukio la kukabidhi Taarifa ya utekelezaji wa Operesheni ya Anwani ya makazi iliyofanyika katika Ukumbi wa Julius Nyerere International Convention Centre Jijini Dar-es-Salaam.
Amesema katika Zoezi la Anwani za Makazi kumejitokeza Changamoto mbali mbali kwa baadhi ya maeneo ambazo zimesababisha kutofanyika ipasavyo kwa zoezi hilo, akitolea mfano wananchi wanaoishi katika maeneo yasiyo rasmi kukaa kisheria. Hivyo ni vyema Wizara husika kutatua changamoto hizo na nyenginezo.
Mhe. Majaliwa ametumia Fursa hiyo kuwataka wananchi kuepuka kukaa maeneo yasiyo rasmi kuishi kisheria ili kuepuka athari mbali mbali zinazoweza kujitokeza.
Sambamba na hayo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewataka viongozi hao kuendelea kuelimisha wananchi juu ya suala zima la umuhimu wa kushiriki katika zoezi la Sensa ya watu na makazi.
Akigusia suala la Mfumo Mhe. Majaliwa ameeleza kuwa Serikali zote mbili zimejipanga kujenga majengo ya kisasa yatakayotumika kwa masuala ya Teknolojia ili kufikia Tanzania ya Uchumi wa Kidigitali.
Kwa upande wake Mwenyekiti Mwenza wa Kamati Kuu ya Kitaifa ya Sensa ya watu na Makazi 2022 Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameeleza kuwa Kukamilika kwa Zoezi la Anwani za Makazi na Postikodi kumetokana na Mashirikiano yaliyopo baina ya Wizara za pande zote mbili za Muungano na kueleza kuwa Mashirikiano hayo yanaongeza Imani kwa viongozi wakuu wa Serikali.
Aidha Mhe. Hemed ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kuwa kukamilika kwa zoezi hilo kutasaidia kukua kwa Uchumi wa Kidigitali Nchini na kufikia Tanzania ya kimaendeleo.
Pamoja na mambo mengine Mhe. Hemed amewataka Wananchi kuendelea kutoa mashirikiano pamoja na kulinda miundombinu iliyowekwa kwa maslahi ya Taifa.
Nae Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape M. Nawiye ameeleza kuwa zoezi la Anwani za Makazi limekamilika kwa Asilimia 95 ambapo kukamilika kwake ni msaada mkubwa uliotolewa na Wakuu wa Mikoa yote Nchini Chini ya Wizara ya Tawala za Mikoa.
Aidha Mhe. Nape ameeleza kuwa Wizara imejipanga kuanzisha Sheria mahususi ya Anwani za Makazi ambayo itasaidia kurahisisha huduma hizo kwa wananchi

