MHE. HEMED AKUTANA NA UBALOZI WA UAE
Kuwepo kwa Ubalozi Mdogo wa Nchi za Falme za Kiarabu hapa Zanzibar kutasaidia kuimarisha uhusiano uliopo baina ya pande zote mbili.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ametoa kauli hiyo alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mdogo wa Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu Zanzibar Mhe. Saleh Ahmed Alhemeiri aliyefika kujitambulisha Afisini kwake Vuga Jijini Zanzibar.
Amesema, mashirikiano ya Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu na Zanzibar ni ya muda mrefu ambapo hatua ya kuanzisha Ubalozi Mdogo hapa Zanzibar kutasaidia kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kwa Maslahi ya nchi hizo.
Amesema, Zanzibar imefurahishwa kwa kuona Balozi huyo anaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Nane (8) ya kuelekeza jitihada zake katika dhana ya Uchumi wa Buluu kwa lengo la kukuza uchumi wake.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amemueleza Balozi huyo kwamba Zanzibar imefungua milango yake kwa wawekezaji mbali mbali kuja kuekeza katika sekta tofauti hapa nchini. Hivyo ametoa wito kwa Umoja huo kutumia fursa hiyo kuja kuekeza.
Aidha, Mhe. Hemed amefurahishwa na hatua ya Balozi huyo kutaka kukaa pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuangalia fursa mbali mbali na kuwasaidia wananchi wa Zanzibar.
Pamoja ya hayo Mhe. Hemed amempongeza Balozi Saleh Alhemeiri kwa kuwa wa kwanza kuteuliwa kushika wadhifa huo na kueleza kuwa uteuzi wake unaonesha uwezo wa kidiplomasia alionao katika nchi yake.
Kwa upande wake Balozi Mdogo wa Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu Zanzibar (U.A.E) Mhe. Saleh Ahmed Alhemeiri amemuhakikishia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa hatua ya kuanzisha Ubalozi Mdogo hapa Zanzibar itasaidia kurahisisha ufanisi wa kazi za kibalozi hapa nchini.
Aidha, amesema UAE ipo tayari kuendeleza ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa lengo la kutimiza malengo ya pande zote mbili.

